-->

Uchaguzi Marekani: Pence na Kaine walumbana kuhusu Trump

Mgombea urais mwenza wa chama cha Republican nchini Marekani Mike Pence na mwenzake wa Democratic Tim Kaine wamelumbana kuhusu taarifa za kodi za Donald Trump kwenye mdahalo wa runinga.. Bw Pence, ambaye ni gavana wa Indiana, amesema mgombea urais wa chama cha Republican Bw Trump alitumia "werevu" katika kutumia sheria za kodi kukwepa kulipa kodi. Lakini Bw Kaine, seneta wa Virginia, alipinga wazo hilo la "werevu" akishangaa iwapo ilikuwa busara kukwepa kulipa pesa za kutumiwa kulipa wanajeshi au kufadhili elimu shuleni. Bw Trump ameshutumiwa sana kutokana na rekodi yake ya ulipaji kodi. Amekataa kufichua taarifa zake za ulipaji kodi lakini gazeti la New York Times majuzi lilifichua kwamba huenda amekwepa kulipa kodi kwa miaka 18 iliyopita. Hili liliwezekana kwa sababu bw Trump, aliyewekeza katika biashara ya ujenzi na uuzaji wa hoteli, alipata hasara kubwa ya zaidi ya $900 milioni mwaka 1995. Hajakanusha habari hizo. Akimshambulia Bw Trump, Bw Kaine alisema: "Nafikiri sote tunaofanya hivyo [kulipa kodi] ni wajinga?"Kaine, 57, alianzisha mjadala huo wenye hisia kali katika chuo kikuu cha Longwood, Virginia kwa kushangaa ni vipi Bw Pence angemtetea Donald Trump. Lakini mpinzani wake wa Republican alimjibu kwa kumkosoa Hillary Clinton kwa kutumia barua pepe yake ya kibinafsi kwa shughuli rasmi pamoja na sera yake ya mambo ya nje ambayo alisema imesababisha vurugu katika baadhi ya maeneo duniani. Mambo mengine makuu: Bw Kaine alitaja makundi ya watu ambao Bw Trump amewatusi, wakiwemo wanawake na wanajeshi waliotekwa vitani Akimjibu Bw Pence amesema Donald Trump amewatusi Wamarekani wachache ikilinganishwa na Bi Clinton Kutumiwa kwa jamii katika shughuli za polisi ndiyo njia muhimu ya kupunguza uhasama baina ya polisi na Wamarekani Weusi, amesema Bw Kaine. Lakini Bw Pence amemtuhumu Bi Clinton kwa kuwafanya polisi waonekane wabaya na kuwatuhumu kuwa wabaguzi wa rangi Wazo la kwamba Donald Trump anaweza kuwa amiri jeshi mkuu "linatutia wasiwasi sana", amesema Bw Kaine Pence amesema yeye na Bw Trump watapunguza kodi inayolipwa lakini bado waweze kulipia huduma za kijamii na afya Sehemu kubwa ya mjadala iliangazia sera ya mambo ya nje. Bw Pence amesema "Marekani si salama sasa" kuliko ilivyokuwa Rais Obama alipochaguliwa na akasema Bi Clinton anafaa kulaumiwa kutokana na kuchipuka kwa kundi la Islamic State. Amesema Rais wa Urusi Vladimir Putin anaweza kumheshimu Trump kwa sababu ya nguvu zake, na mgombea wake. "Hilo ni wazi". Msema kweli: Mdahalo wa Clinton na Trump Lakini Bw Trump amewasifu pia viongozi wa kiimla, amesema Bw Kaine, na watu anaowaenzi ni Bw Putin, kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong-un na kiongozi wa zamani wa Libya Muammar Gaddafi. Mdahalo huo ulisimamiwa na mtangazaji wa CBS News Elaine Quijano.

Nemo enim ipsam voluptatem quia voluptas sit aspernatur aut odit aut fugit, sed quia consequuntur magni dolores eos qui ratione voluptatem sequi nesciunt.

Disqus Comments